Na Jumia Travel Tanzania
Miongoni
 mwa tasnia zinazokua kwa kasi sasa hivi nchini Tanzania ni uandishi wa 
mtandaoni au blogu. Kuenea na ukuaji wa matumizi ya mtandao wa intaneti 
kumepelekea watu waliokuwa wanatamani kuingia kwenye tasnia ya uandishi 
kufungua blogu zao mitandaoni.
Blogu
 zinatoa fursa kubwa kwa watu mbalimbali wanaopenda uandishi kuandika 
masuala mbalimbali juu ya mada tofauti na kuwashirikisha wasomaji wao 
kwa njia ya mtandao. Jumia Travel ingependa
 kukufungua macho kwamba miongoni mwa masuala ambayo mpaka sasa 
hayajaangaziwa kwa kiasi kikubwa ni pamoja na vivutio vilivyopo sehemu 
tofauti za nchi ya Tanzania. Zifuatazo ni baadhi tu ya faida chache za 
kuanza kuandika na kuwashirikisha wasomaji wako juu ya maeneo tofauti 
unayoyatembelea.   
Ni fursa ya kuwashirikisha wasomaji wako sehemu tofauti ulizotembelea. Sio
 watu wote wamebahatika kusafiri na kujionea maeneo tofauti mbali na 
pale wanapoishi. Zipo sababu nyingi zikiwemo shughuli zao kutowaruhusu, 
kutokuwa na kipato kinachokidhi au kuwa na majukumu mengine. Hivyo basi 
kama umepata fursa ya kusafiri sehemu mbalimbali kuna haja ya 
kuwasimulia wale ambao hawajawahi kufika. Kwa kufanya hivyo utajikuta 
bila ya kujijua unatoa elimu, kutoa mwamko na hamasa ya watu juu ya 
sehemu hiyo na hata kutembelea siku za usoni. 
Kunaweza kuwa chanzo cha kukuingizia kipato.
 Unaweza ukaanza kama masihara kuwa unaandika juu ya sehemu 
unazotembelea kwa kuwa unapenda lakini huweza kujua kwamba inawezekana 
kuna watu wanafuatilia kazi zako na kuzipenda. Matokeo ya kuwa mwandishi
 mzuri wa makala za kuvutia na wasomaji wako wakazipenda kunaweza 
kukufungulia milango ya biashara. Kampuni au mashirika mbalimbali 
yanaweza kupendezewa na kazi zako na kutaka kuzitumia au wakakulipa ili 
uandike kwa ajili yako. Kwa nchi ambazo zimeendelea hususani za Ulaya, 
Marekani na Asia wapo waandishi wengi wa namna hii wanasafiri na 
kuandika vile wanavyoviona na kujiingizia kipato cha kutosha na 
kuendesha maisha yao. Mbali na njia hiyo yapo pia makampuni, mashirika 
au wafanyabiashara watakaokutafuta kutaka kutangaza kupitia blogu yako. 
Kenya wenzetu wamekwishaanza na wanafanyaa vizuri hivyo ni wakati sasa 
kwa watanzania nao kuchangamkia fursa hii.    
Blogu yako inaweza kutumika kama sehemu ya kutoa elimu.
 Ukiwa ni mwandishi mzuri na uliyobobea kwenye sekta unayoiandikia kuna 
fursa kubwa ya kujijengea uaminifu na mamlaka kwa wasomaji wako. 
Ukishajijengea uaminifu miongoni mwa wasomaji wengi basi unakuwa na 
mamlaka juu ya kile unachokiandikia na hivyo blogu yako ikatumika kama 
kielelezo muhimu. Kwa hiyo ili kufanikiwa katika hili hakikisha kwamba 
unaijua vema sekta uliyopo ili kutoa taarifa ambazo watu wataziamini na 
kuzitumia.
Uandishi wa kwenye blogu ni miongoni mwa taaluma yenye soko kubwa kwa sasa. Katika
 ulimwengu huu wa kidigitali hakuna taasisi, shirika, kampuni au 
mfanyabiashara ambaye hayupo mtandaoni. Na hii ni kutokana na uwezo wa 
njia hiyo kuwafikia watu wengi na tofauti kwa haraka ndani ya muda 
ukizingatia hakuna gharama kubwa zinazotumika. Hivyo basi kwa kuonyesha 
uwezo wako wa kuandika unaweza kupata fursa ya kutafutwa na makampuni 
yenye uhitaji na watu wenye sifa kama zako. Hivyo basi ni vema kuonyesha
 bidii na ueledi mkubwa kwenye kile unachokiandika ili kuwavutia watu 
makini.    
Ni fursa ya kuitangaza nchi yako.
 Bila ya kujijua kwamba kupitia maandiko juu ya sehemu mbalimbali 
unayoyachapisha kwa wasomaji wako yanaweza kuwa na mchango mkubwa kwenye
 kuvitangaza vivutio vya nchi yako. Mwisho wa siku simulizi za maeneo 
unayokwenda huwavutia watu wa ndani na nje ya nchi na kutamani kwenda 
kujionea wenyewe kwa macho yao. Lakini isingekuwa hivyo bila ya nguvu ya
 ushawishi wa makala zako. Hivyo ni vema kuandika kwa ustadi mkubwa 
ambao utamfanya mtu akisoma ajikute naye ni sehemu ya safari 
uliyoipitia.
Kuna
 matukio mengi sana ya kuvutia na kusisimua ambayo tunajionea sehemu 
mbalimbali tunazozitembelea ambayo kwa hakika kuwasimulia marafiki pekee
 haistoshi. Jumia Travel inaamini kwamba kuanzisha blogu yako unaweza 
kuushirikisha ulimwengu na kusafiri nawe sehemu mbalimbali za Tanzania. 
Ni rahisi, haichukui muda na hakuna malipo ili kufungua blogu, tembelea 
tovuti kama vile Blogger au Wordpress ambayo inaweza kukuwezesha kufungua blogu yako bure kabisa.

Comments
Post a Comment