Na Jumia Travel Tanzania
Mitandao
 ya kijamii ni huduma zinazopatikana kwenye intaneti ambazo 
zinakuwezesha kuwasiliana, kutengeneza maudhui na kuwashirikisha watu 
wengine waliopo mitandaoni. 
Tofauti na watu wanavyoitumia, Jumia Travel
 ingependa kukufunua macho kwamba mitandao ya kijamii imeleta fursa 
kubwa ya kutangaza biasahara za aina mbalimbali. Unaweza kuitumia 
mitandao hiyo kwa kufanikisha malengo kama vile; kukuza jina na biashara
 yako, kuwafahamisha wateja juu ya bidhaa na huduma zako, kujua wateja 
wanaichukuliaje biashara yako, kuwavutia wateja wapya pamoja na kujenga 
mahusiano thabiti na wateja ulionao. 
Faida za kutumia mitandao ya kijamii
Kuwafikia watu wengi.
 Badala ya kutegemea wateja kuja moja kwa moja ofisini kwako mitandao ya
 kijamii huwafikia mamilioni ya watu sehemu mbalimbali ndani ya muda 
mfupi. 
Kuwafikia wateja unaowakusudia.
 Uzuri wa mitandao ya kijamii ni kwamba hutofautiana kwa aina ya 
watumiaji wake kama vile vijana, watu wazima, wanasiasa, wanataaluma na 
matabaka mengine. Hivyo hii hutoa fursa kwa mfanyabiashara kulingana na 
huduma au bidhaa aliyonayo kujiwekea mkakati wa namna ya kuwafikia.
Unafuu.
 Haikuhitaji kuwa na fedha ndipo ufungue akaunti kwenye mtandao wa 
kijamii mara nyingi ni intaneti tu. Lakini kama unataka kuitumia kwa 
malengo ya kibiashara wamiliki wake hutoza kiasi kidogo cha fedha 
ambacho ni rahisi kukimudu.
Kumfikia mtu binafsi.
 Mitandao ya kijamii inakuruhusu kujenga ukaribu au kuwasiliana na 
wateja wako kwa ukaribu zaidi. Uwezo wa kuyapokea na kuyajibu maswali 
yao au kuyasikiliza na kuyafanyia kazi maoni yao vina ushawishi mkubwa 
katika kuwafanya wateja kutumia huduma na bidhaa zako.
Uharaka. Ndani ya muda mfupi unaweza kusambaza taarifa juu ya huduma na bidhaa zako kwa watu wengi kwenda sehemu mbalimbali.
Urahisi. Haikuhitaji
 kuwa na ‘madigrii’ ya vyuo vikuu ili kuweza kutumia mitandao ya 
kijamii. Ni rahisi kuitumia kwa njia mbalimbali kama vile kompyuta, 
tabiti au simu za mikononi ambazo watu wengi wanamiliki.   
Mitandao mikuu ya kijamii unayoweza kuitumia
Facebook.
 Mtandao huu hutoa fursa nzuri kwa wafanyabiashara kuwasiliana na wateja
 wao moja kwa moja, kuweka picha na video, kutangaza ofa walizonazo, 
bidhaa na huduma mpya na mambo mengine.
Twitter.
 Mara nyingi huduma hii hutumika kutuma na kupokea jumbe fupi kutoka kwa
 wateja wapya na waliopo. Siku hizi pia hutumika kama nyenzo muhimu kwa 
kuweka viungo ambavyo vitawapeleka wasomaji kwenye tovuti. 
Youtube.
 Mtandao huu hutumika kwa kuweka video tofauti, zinaweza kuwa juu ya 
huduma na bidhaa ulizonazo, namna ya kuzitumia pamoja na taarifa 
mbalimbali ili wateja wako wazitazame.
Blogu.
 Kama mfanyabishara pia unaweza kufungua mtandao huu utakaokupatia fursa
 kubwa ya kuwashirikisha wasomaji wako juu ya huduma na bidha zako 
pamoja taarifa mbalimbali.
Instagram. Mbali
 na mtandao huu ipo mingine pia inayowawezesha watumiaji kuweka na 
kuwashirikisha watu wengine picha mbalimbali. Kwa mfano hivi karibuni 
Instagram wameuboresha mtandao wao kwa kuwawezesha watumiaji wake kuweka
 picha zaidi ya moja. Hivyo kutoa fursa nzuri kwa wafanyabishara kuweka 
picha mbalimbali za bidhaa na huduma zao.
Mbali na kuwepo kwa faida lukuki za mitandao ya kijamii, Jumia Travel
 ingependa kukuasa kwamba bado unahitajika umakini mkubwa katika nanma 
ya kuitumia. Miongoni mwa changamoto unazoweza kukumbana nazo ni pamoja 
na kupoteza muda na fedha zako kwa kuwekeza kwenye  kitu ambacho 
hakitoleta faida, kusambaa kwa habari zisizo sahihi kuhusu biashara yako
 kwa wateja na kukumbana na matatizo ya kisheria endapo usipofuata au 
kuvunja taratibu zilizowekwa na mamlaka husika.

Comments
Post a Comment